Imeandikwa na İrem Berna Güvenç Erdoğan, Middle East Technical University, Turkey; Iga Palacz-Poborczyk, SWPS University, Poland; Olga Perski, Stockholm University, Sweden; Sheson Tiwari, Psyfolks Education, India; Belgin Ünal, University of Michigan, USA
Maendeleo ya COVID 19 na umuhimu wa kupata matibabu mapema
Watu wengi hupona kutokana na COVID 19 bila kuhitaji matibabu ya kina hospitalini. Huduma ya kawaida na tiba ya kupunguza dalili huwa inatosha. Hata hivyo, kuna kundi la watu hasa wazee, watu ambao hawajachanjwa, na wale wenye magonjwa sugu ambao wako kwenye hatari kubwa ya kupata ugonjwa mkali. Ndiyo sababu, Shirika la Afya Duniani WHO linasisitiza umuhimu wa kutoa matibabu mapema kwa makundi haya ili kupunguza uwezekano wa kulazwa hospitalini, kuhitaji uangalizi maalum, au hata kifo.
Kwa baadhi ya wagonjwa, dawa za antiviral hupendekezwa ili kupunguza kwa kiasi kikubwa hatari ya kupata ugonjwa mkali, na huwa na ufanisi zaidi zikianza kutolewa ndani ya siku tano za mwanzo tangu dalili kuanza. Kuchelewa kupima, kuchelewa kupata utambuzi, au kuchelewa kuanza matibabu hupunguza sana ufanisi wa dawa hizi. Kwa hivyo, kuhakikisha upatikanaji wa huduma za afya kwa haraka hasa katika ngazi ya jamii ni muhimu ili kuongeza manufaa ya matibabu na kuboresha matokeo ya mgonjwa.
Ushahidi wa kimuktadha unaoonyesha umuhimu wa matibabu ya mapema katika kupunguza kulazwa hospitalini na vifo
Matibabu ya mapema hupunguza kwa kiasi kikubwa hatari ya kulazwa hospitalini na vifo, hasa kwa wagonjwa walio kwenye hatari kubwa ya kupata ugonjwa mkali. Ili kuelewa umuhimu wake, ushahidi wa utafiti lazima uangaliwe kulingana na mazingira ya kitabibu na ya idadi ya watu.
Katika utafiti mkubwa wa kimataifa uliofanyika Marekani, Brazil, Afrika Kusini, India na Mexico, watu wazima walio katika hatari kubwa, ambao hawakulazwa na hawakuchanjwa, walipopata dawa za antiviral ndani ya siku tatu za kwanza za dalili, walikuwa na uwezekano mdogo kwa karibu asilimia 89 wa kulazwa hospitalini au kufa ikilinganishwa na waliopata placebo.
Vivyo hivyo, matibabu ya mapema kwa kutumia Sotrovimab aina ya kingamwili maalum yameonyesha kupunguza hatari ya kuendelea kwa ugonjwa kwa asilimia 85 wakati wa awamu za mwanzo za virusi ufanisi ulitofautiana baadaye. Hii inaonyesha umuhimu wa kuingilia mapema kwa watu walio kwenye hatari, wakiwemo wazee na wale wenye magonjwa kama unene kupita kiasi au kisukari. Zaidi ya asilimia 60 ya washiriki walitoka katika jamii za Hispanic na Latinx, ambazo zilipata athari kubwa wakati wa janga, jambo linaloonyesha kuwa matibabu ya mapema yanafaa katika makundi mbalimbali ya kijamii.
Aidha, tafiti 18 za dunia kutoka nchi mbalimbali yalionyesha kuwa matibabu ya mapema yalipunguza kwa kiasi kikubwa kulazwa hospitalini na vifo, na manufaa yalikuwa makubwa zaidi matibabu yalipoanza ndani ya siku tano za dalili. Utafiti mkubwa kutoka Hong Kong uliowafuatilia zaidi ya wagonjwa 87000 ulibaini kuwa kuanza matibabu ndani ya siku 1 hadi 2 tangu dalili kuanza kulipunguza kwa kiasi kikubwa kulazwa na vifo ikilinganishwa na kuanza baadaye. Mwelekeo huu ulionekana katika makundi mbalimbali ya umri, jinsia na hali ya chanjo.
Kwa ujumla, ushahidi unaonyesha jambo moja muhimu: matibabu ya mapema hufanya kazi, na kuchelewa hupunguza ufanisi wake.
Muhtasari wa tiba zinazopendekezwa kulingana na miongozo ya kitabibu ya ndani
Kwa kuwa muda wa kuanza matibabu ni muhimu, ni tiba zipi zinapatikana, na nani anapaswa kuzipata?
Kwa watu wazima ambao hawajalazwa na wana COVID 19 ya kiwango cha chini hadi cha kati, dawa za antiviral ndizo zenye ufanisi zaidi. Kwa sasa kuna dawa tatu zinazotumika sana: Remdesivir, Nirmatrelvir Ritonavir Paxlovid, na Molnupiravir. Uchaguzi sahihi hutegemea hatari ya mgonjwa, dawa anazotumia, njia ya utoaji, na upatikanaji wa dawa.
Remdesivir hupewa kwa njia ya mshipa kwa siku tatu mfululizo na hupendekezwa pale ambapo dawa za kumeza hazifai. Katika utafiti wa wagonjwa , kozi ya siku tatu ilipunguza kwa kiasi kikubwa kulazwa na vifo. Pia hupendekezwa wagonjwa waliolazwa wanaohitaji oksijeni, pamoja na dawa za kupunguza uchochezi, na kama chaguo la pili kwa wagonjwa wa nje walio kwenye hatari kubwa pale Paxlovid inapofaa.
Nirmatrelvir Ritonavir Paxlovid hupewa kwa njia ya kumeza kwa siku tano na imeonyesha kupunguza kwa kiasi kikubwa hatari ya kulazwa na vifo kwa watu walio kwenye hatari kubwa. WHO inapendekeza Nirmatrelvir/Ritonavir kama chaguo la kwanza kwa wagonjwa ambao hawajalazwa hospitalini na walio kwenye hatari kubwa.
Molnupiravir ni dawa ya kumeza inayopendekezwa kama chaguo la tatu kwa wale wasioweza kupata au kuvumilia dawa nyingine. Utafiti umeonyesha kupunguza kulazwa na vifo kwa watu wazima ambao hawakuchanjwa, ingawa ushahidi kwa waliochanjwa unaonyesha matokeo yasiyolingana kupendekeza manufaa madogo zaidi.
Upatikanaji wa dawa hutofautiana kulingana na mfumo wa afya na rasilimali. Kwa dawa zote tatu, kuanza mapema ni muhimu, kwani ufanisi hupungua kadri ugonjwa unavyoendelea. Kicheleweshaji chochote kupima, utambuzi, au kuandikiwa dawa hupunguza nafasi ya kupata manufaa.
Mbinu za mawasiliano kwa wagonjwa ili kupunguza kusitasita kuanza matibabu
Kwa nini watu bado husita kuanza matibabu, hata kama ushahidi unaonyesha manufaa yake?
Sababu kadhaa huchangia kuchelewa kufanya maamuzi. Kikwazo cha kawaida ni mtazamo wa “ngojea uone,” ambapo mgonjwa hudharau ukali wa COVID 19 na kuchelewesha matibabu. Wasiwasi kuhusu madhara ya dawa au mwingiliano na dawa nyingine pia ni wa kawaida, hasa kwa wagonjwa wanaotumia dawa nyingi.
Zaidi ya hayo, uelewa mdogo na ugumu wa kupata taarifa sahihi huchelewesha hatua za haraka. Tafiti zinaonyesha kuwa ni asilimia 54 tu ya watu wazima waliowahi kusikia kuhusu dawa kama Paxlovid (Nirmatrelvir/Ritonavir) kabla ya kugunduliwa na COVID 19. Haya yote huongeza mashaka na kusababisha kusitasita kupata matibabu.
Nini kinaweza kufanywa tofauti?
- Sisitiza kuwa matibabu ya COVID 19 ni hatua za kuzuia ugonjwa kuwa mbaya, si tu kupunguza dalili. Eleza kuwa dawa za antiviral hulenga kuzuia ugonjwa kali, kwa hivyo wagonjwa wanaelewa kuwa matibabu ya mapema hupunguza hatari ya ugonjwa mbaya na kulazwa hospitalini.
- Mapendekezo ya moja kwa moja kutoka kwa mtoa huduma anayemfahamu mgonjwa ni muhimu. Wagonjwa hukubali matibabu kwa urahisi zaidi wakipewa ushauri wa moja kwa moja na daktari wao. Takwimu zinaonyesha kuwa utayari wa kutumia dawa huongezeka kwa zaidi ya asilimia 20 wakishauriwa na daktari kufikia hadi 93% ya kukubalika kati ya watu wazima wenye umri wa miaka 65 na zaidi.
- Ufuatiliaji wa mapema na elimu ya kawaida ni muhimu. Wagonjwa wachache sana huomba matibabu wenyewe; chini ya asilimia 20 ya wanaostahili huwa na taarifa za kutosha na ujasiri wa kuuliza. Timu za afya zinapaswa kuwasiliana na wagonjwa wanaostahili mara tu baada ya utambuzi na kuwapa taarifa fupi, wazi na za moja kwa moja.
Mambo muhimu ya kukumbuka
- Matibabu ya mapema ndani ya siku tano za dalili ni muhimu kwa watu walio kwenye hatari kubwa, na hupunguza kwa kiasi kikubwa kulazwa hospitalini na vifo.
- Dawa za antiviral kama Paxlovid, Remdesivir na Molnupiravir zina ufanisi zaidi zikianza mapema.
- Licha ya manufaa yake, kuchelewa bado hutokea kutokana na uelewa mdogo na kusitasita.
- Mapendekezo ya haraka kutoka kwa watoa huduma, ufuatiliaji wa mapema, na kueleza dawa kama hatua za kuzuia ni muhimu kuongeza matumizi na kuboresha matokeo ya afya.
Mapendekezo ya vitendo
- Pendelea kuanza matibabu mapema.
Dawa za antiviral zina ufanisi zaidi ndani ya siku tano za dalili. Hakikisha wagonjwa walio kwenye hatari wana vifaa vya kupima nyumbani na wanajua kuwasiliana siku ile ile wanapopata majibu chanya.
- Lenga walio hatarini zaidi.
Watu wenye kisukari, magonjwa ya moyo, figo sugu, au BMI zaidi ya 30 mara nyingi hujisikia sawa mwanzoni, lakini wako kwenye hatari kubwa ya kuzorota ghafla.
- Tambua na uchunguze mapema.
Pitia orodha za wagonjwa ili kubaini walio kwenye hatari na kuweka utaratibu wa haraka wa utambuzi.
- Weka mtazamo wa kinga.
Eleza kuwa lengo si kutibu kikohozi cha leo, bali kuzuia kulazwa wiki ijayo.
- Punguza ucheleweshaji wa kuandikia dawa.
Kagua dawa anazotumia mgonjwa na vigezo vya kustahili mapema ili kurahisisha kuanza matibabu ndani ya muda muhimu.
Imetafsiriwa na Mercy Mukoya